MSHINDE GOLIATHI.
- Mch. Gasper Madumla
- Aug 26, 2014
- 2 min read

Bwana Yesu asifiwe…
Kwa ufupi;
Goliathi alikuwa ni mtu wa vita wa kifilisti. Habari za mtu huyu zimekuwa maarufu sana baada ya kuuwawa na Daudi. Hii inaonesha kushindwa kwake katika mapambano makali kulimfanya ajulikane. Na ndivyo ilivyo hata leo,wapo watu ambao ni maadui zako wasiofahamika,lakini watafahamika tu pale utakapowashinda. Kijana mdogo Daudi alimshinda Goliathi mtu hodari wa vita kama mchezo fulani wa kuigiza. Hakika ulikuwa ni muujiza kwa watu wengi kwa watu wengi pale shujaa wao Goliathi alipouwawa kwa sababu hawakutegemea kabisa kwamba kuna siku moja huyo shujaa atakufa.
Hata leo;watu wanapowaangalia maadui zao ambao ni mashujaa kwa uadui,hudhania kwamba wataishi milele bila kujua ya kwamba kuna siku watakufa tena sio kifo cha kawaida bali wataangamizwa kabisa ikiwa kama wataendelea kuwafuata fuata watu wa Mungu.Hata huyo adui yako wa leo,kuna siku hutamwona tena kwa maana Bwana atakupigania. Ukiyasoma maisha ya Daudi,utashangaa sana kwa maisha aliyokuwa nayo;
kwa maana kwanza Daudi alikuwa ni mtoto wa nane wa mzee Yese (tena ni mtoto wa kambo),aliyedharauliwa na ndugu zake. Lakini ndani ya Daudi kulikuwa na moyo unaompendeza Mungu,naye akakua katika malezi ya kuchunga mifugo ya baba yake mzee Yese. Bila shaka Daudi hakujua kwamba alikuwa akiandaliwa ushupavu,ujasiri; kwa maana akiwa nyikani alikuwa akipambana na wanyama wakali kama vile dubu,na kuwashinda!
Daudi akutana na Goliathi.
Siku moja Daudi alikutana na Goliathi aliyeyatukana majeshi ya Israeli. kwa kuwa moyo wa Daudi ulikuwa umeandaliwa na Mungu kikamilifu,hivyo hakuweza kuchukuliana na matusi ya huyu mfilisti asiyetahiriwa. “Wivu wa Bwana” ukamla Daudi,naye hakuweza kutulia alipoona dhihaka ya juu ya Mungu aliye hai. Kwako; itafika wakati ambao utaonana na Goliathi wako mwenye dhiaka,lakini swali la kujiuliza Je wivu wa Bwana utakula ndani yako?
Au utacheka cheka tu bila kuchua hatua ya kumnyamazisha kiimani? Si kwa kupigana kimwili bali kiroho,Ikiwa Kristo U ndani yako,huna budi kumnyamazisha huyo Goliathi kama alivyofanya Daudi kijana mdogo lakini ana Mungu ndani yake. ( Goliathi wako wa leo,ni yeyote yule ambaye kwako amekuwa ni mtu wa dhiaka,adui,mzuiaji wa mambo ya Mungu kwako,mchawi n.k )
Hakuna mtu aliyekosa kuwa na Goliathi,lakini tatizo lipo ni kwa namna gani utafanikiwa kumshinda? Jifunze kwa Daudi mtu ambaye alimkabidhi Goliathi kwa Bwana. Na Bwana akanunua vita,vita ikawa si ya Daudi bali ni ya Bwana ( 1 Samweli 17:47). Hii ndio njia kubwa na maana ya kushughulika na adui yako,ni pale unapomkabidhi kwa Bwana alafu Bwana atamshughulikia. Fikiri hili lifuatalo;
Je kama Daudi angemwendea Goliathi kwa silaha za mwili,kama alizofalishwa na Sauli,angeweza kumpiga Goliathi?
Ukweli ni kwamba Daudi asingeliweza kumshinda Goliathi isipokuwa Bwana alikuwa pamoja na Daudi. Na ndio maana Daudi hakuwa na haja ya kutumia silaha za kawaida bali silaha za Mungu. Vipi wewe,? Pale unapoinukiwa na adui yako,unatumia nini? Je unatumia panga,maneno au kumshtaki kwa polisi? Ukifanya hizi,ujue utakuwa ukipigana kimwili,nawe utapigwa upigike! Tumia silaha za kiroho kama maombi,neno n.k napo utamshinda huyu adui.
Ikiwa kama umebarikiwa nifahamishe, pia Kwa maombi na msaada zaidi , piga +255 683 877 900.
What’sapp namba .+255 746 446 446
Mch. G. Madumla.
UBARIKIWE.
Комментарии