top of page

MAOMBI / PRAYERS~10


Mch Madumla

Na mch.Gasper Madumla


03.NI JINSI GANI YA KUOMBA IPASAVYO?

Kwa ufupi..

Ukweli ni kwamba sote hatujui kuomba ipasavyo isipokuwa Roho hutusaidia udhaifu wetu (Warumi 8:26). Hivyo basi hakuna mtu anaweza kusema kwamba yeye ni mtaalumu wa maombi au fundi wa maombi pasipo kuwezeshwa na Roho mtakatifu. Roho mtakatifu ndio hutuwezesha kuomba ipasavyo,hatuna budi kumjua na kujifunza habari zake kwa usahihi.

Tatizo kubwa linalotukwamisha katika maombi yetu,ni kwamba wengi si wasomaji wa neno la Mungu tena hatulitafakari Neno. Sasa,ikiwa wewe si msomaji na huna neno la Mungu ndani yako; basi ujue hutaweza kuomba ipasavyo,kwa maana itafika wakati utakosa maneno ya kutamka. Neno la Mungu linaufanya moyo wako kusheheni Neno kiasi cha kuwa na mafunuo mengi,na mtililiko wa maombi.

Laiti kama tungelikuwa tunamtumia ipasavyo Roho  mtakatifu katika maombi yetu,basi ni dhahiri tungelikuwa tuna majibu katika yale tuyaombayo. Hatua zifuatazo zinafaa sana pale unapoingia katika maombi ya aina yoyote ile(Lakini sio kanuni bali ni vyema sana ukatumia hatua hizi uombapo). Hivyo basi zipo hatua tatu muhimu sana katika maombi yako,nazo ni;

i) Kushukuru~ Kabla hujaanza kuomba ombi lako,basi ni vyema ukaanza kumshukuru Bwana Mungu wako hata kwa nafasi tu uliyoipata ya maombi,kwa maana wengine walitamani wapate nafasi kama yako lakini hawakupata,Je wewe ni nani hata upate nafasi ya maombi lakini pia tafakari mema aliyokutendea, Hivyo unapaswa kuanza na shukrani.

“ Haleluya.Mshukuruni BWANA kwa kuwa ni mwema,Kwa maana fadhili zake ni za milele.” Zab.106

ii) Toba / rehema.~ Ni muhimu kujishusha mbele za Mungu na kujiona kuwa wewe ni mkosefu ili utubu sasa. Maombi haya ni muhimu sana ili kusudi utengeneze kwanza na Bwana kabla ya kuendelea mbele zaidi.

Wapo baadhi ya wapendwa wameisukumia mbali imani ya toba,wakidai kwamba hakuna haja ya kutubu mara kwa mara maana toba walioifanya siku ya kuokoka kwao inatosha.Mtazamo wa namna hii ni hatari sana,kwa maana ni ukweli usiopingika kwamba twajikwaa mara kwa mara,hivyo ni vyema hata kama umeokoka basi usijihesabie haki.

 Lakini ukawa huoni mpenyo wa uponyaji kwa sababu ya uwepo wa dhambi,kwa sababu chanzo cha magonjwa mengi ni dhambi ndani ya mtu.Ndio maana mtunga Zaburi amesema “  Akusamehe maovu yako yote,Akuponya magonjwa yako yote,” Zab.103:3, ;

hii ikiwa na maana kwamba unaposamehewa dhambi zako basi ujue uponyaji ni mali yako. Hata unapoenda kumuombea mtu,hakikisha unamuongoza sala ya toba,mtubishe vizuri ili uponyaji uanze kuumbika.

iii)Kuomba msaada wa Roho mtakatifu.~ Ni muhimu ukaomba msaada wa Roho mtakatifu ili akusaidie kuomba ipasavyo. Akupe wepesi wa maombi yako na akuwezeshe kwenye kila eneo. Hapo sasa waweza kuendelea na maombi yako uliyopanga.

MAZINGIRA YAFAAYO KATIKA MAOMBI.

Ilikuwa siku moja  jioni nilipokuwa nikitoka kazini (maana niliajiriwa kabla ya kuwa mchungaji) nikapata msukumo wa kumuombea mdogo wangu aliyekuwa Afrika ya kusini. Siku hiyo Roho alinisukuma nipambane na kila roho ya uadui iliyomuinukia.

Kumbe siku hiyo hiyo naye alikuwa yupo katika kona mbaya ameachwa na mwenyeji wake,hajui cha kufanya na hana pesa yoyote wala hakuwa na simu, kwa ufupi; alikosa msaada wa kibinadamu.

Nami nikaomba saa ile ile,kisha Bwana alifanya njia kwa ndugu yangu akapata msaada. Nikajifunza kumbe muda wa maombi ni sasa sio kesho,pale unapopata mzigo/msukumo wa maombi ndio hapo hapo pa kuomba.

Hivyo;Ninapozungumzia mazingira yanayofaa kwenye maombi nina maana ya maeneo gani mazuri utakayoyatumia wakati wa maombi yako. Lakini awali ya yote ni lazima tujue kwamba Roho mtakatifu hana mipaka wala hafungwi kwa mazingira yoyote yale. Tukilijua hilo litatusaidia sana haswa tunapoyaangalia mazingira ya maombi.

▪Eneo zuri lifaalo katika maombi ni mahali popote pale ambapo ndani yako unapata msukumo wa maombi.~ Inawezekana ukawa katika kiwanja cha mpira wa miguu mahali ambapo kuna fujo za kila aina,lakini eneo lilo hilo ndipo  gafla unapata msukumo wa maombi,basi ukiona hivyo ujue huo ndio muda muafaka wa kuingia katika maombi pasipo kuangalia mazingira uliyopo. 

Mfano mwingine;Unaweza ukawa upo toilet/msalani, lakini gafla ukapokea mzigo wa maombi,basi ujue unatakiwa uingie katika maombi saa hiyo hiyo bila kuchelewa na ikiwa hujui utaomba nini,anza kumuuliza Roho mtakatifu,Naye atakupa cha kuombea,kwa maana Yeye ni mwaminifu Naye husema hata leo.

Wakristo wengi wamekwama katika eneo hili,kwa sababu pale wapatapo mzigo wa maombi wengi hawahushughulikii kikamilifu kwa muda uliotolewa, bali wengi husubiri wafanye kwa muda wao. Ikiwa utapokea ujumbe wa kufanyia kazi leo,nawe ukaupuuzia kisha ukapanga siku nyingine ya kuushughulikia basi ujue itakughalimu sana.

Ni kama vile ukipewa chakula kisha usile leo ukakiacha mpaka siku nyingine labda siku tatu zijazo au wiki moja ijayo ndio ule,basi ujue kitakuwa kipolo kilichoharibika. Viporo vingine utavipasha moto,lakini vingine havipashiki. 

Ukiwauliza watu wengi waliopata mzigo wa kuomba kisha wakapuuzia watakuambia madhara waliyoyapata. Ndiposa nikagundua kwamba;hatujui muda muafaka wa kuomba tena wengi hatujui ni mazingira gani yatupasayo kuongea na Mungu. Jifunze kwa Hezekia mtu aliyepewa taharifa ya kutengeneza mambo ya nyumba yake kwa maana atakufa. Biblia inatuambia Hezekia aliomba pale alipopata ujumbe(Isaya 38:1-6). 

Hivi,jiulize Hezekia angelifanya kama wengi wafanyavyo leo kupuuzia ujumbe wa Mungu,alafu labda angelisema “Aah,nitamkumbusha Mungu kesho...” Unafikiri angelipona? Au ingelikuwaje? Kumbe yafaa kuomba saa ile ile penye ujumbe wa Mungu,au penye msukumo.

~Hivyo mazingira ya Roho si mazingira ya kwako,ratiba zake si ratiba zako. (Lakini ni ukweli kwamba tunazo ratiba zetu tulizojiwekea za kukutana na BWANA MUNGU kwa njia ya maombi.)

Ikumbukwe;

kila eneo limebeba hali yake ya kiroho. Mfano;hali ya kiroho iliyopo nyumba za wageni/gesti ni tofauti kabisa na hali ya kiroho ya kanisani. Hivyo ratiba za maombi mazuri zinapaswa kukamilishwa katika mazingira yafuatayo;

(i) Kanisani;

Watu wawili walipanda kwenda hekaluni kusali, mmoja Farisayo, wa pili mtoza ushuru.” Luka 18:10

Kanisani ni eneo la utulivu sana,mahali pa kukutana na Bwana. Eneo hili la hekalu limejaa upako usio wa kawaida,kwa maana ardhi ya kanisa haijabeba laana bali baraka. 

(ii)Kambi za maombi.

Ni eneo maalumu lililotengwa kwa ajili ya maombi,siku zote huwa ni eneo la faragha mbali na maeneo ya nyumbani. Yesu nae mara nyingi alitumia muda wake kujitenga na wengine,kisha kupanda mlimani ili kuomba; “ Naye alipokwisha kuwaaga makutano, alipanda mlimani faraghani, kwenda kuomba. Na kulipokuwa jioni, alikuwako huko peke yake.” Mathayo 14:23

(iii) Nyumbani eneo la faragha.

Eneo la nyumbani kwako pia linafaa kwa ajili ya kufanyia maombi. Lakini tafuta sehemu tulivu mahali ambapo hakuna usumbufu wa makelele ya muziki au purukushani zozote. Angalia jinsi ambavyo nyumbani kwa Mariamu palivyotumika kwa ibada za maombi 

Na alipokuwa akifikiri haya akafika nyumbani kwa Mariamu, mamaye Yohana, ambaye jina lake la pili ni Marko; na watu wengi walikuwa wamekutana humo wakiomba. ” Matendo 12:12

Kwa huduma ya maombezi piga sasa; +255 683 877 900

What’s app +255 746 446 446

ITAENDELEA…

Mchungaji G.Madumla.

UBARIKIWE.

Comments


Post: MAFUNDISHO

Follow

  • Facebook
  • Twitter

©2022 by MAFUNDISHO YA NENO LA MUNGU. Proudly created with Wix.com

bottom of page