top of page

KUKUA KIROHO ? ~02


Mch.Madumla.

Mchungaji Gasper Madumla.


Bwana Yesu asifiwe…

Kumbuka sehemu tulikoishia kujifunza,tuliishia kuangalia tunda la Roho. Na nikajiuliza ~Je nitawezaje kuvikwa tunda hili la Roho?( yaani upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole,na kiasi; ).

Jibu;

Tunda la Roho ni matendo ya Roho yaliyo juu ya sheria. Hivyo kwa sababu mwenye matendo haya ni Roho mwenyewe (Roho mtakatifu ),naye ndie atoae kama apendavyo. Tunda la Roho linaanzia kuvikwa tangu siku ile ulipotia ufahamu kuzichukia dhambi kwa toba na kumpokea BWANA YESU (kuokoka).

Katika siku ya kwanza ya wokovu,mtu huvikwa tunda hili kama mbegu ndogo ya haradali,ambapo mtu huyu akiendelea kudumu katika imani aliyoipokea,tunda la Roho nalo hukua na kuchukua nafasi moyoni mwake.

Tazama mtu alikuwa ni mwenye huzuni,lakini alipookoka chembe ya furaha ikaingia kwa mtu huyo. Na ikiwa ataendelea kudumu katika wokovu,huzuni hutoweka na hatimaye furaha ya kweli inachukua nafasi,sasa furaha ni sehemu ya tunda la Roho. 

Au tazama mtu aliyekuwa ni mwenye kujawa na chuki. Lakini alipookoka siku za kwanza kwanza,taratibu chuki huondoka yanyewe,kisha na kuanza kupenda,tena upendo ni sehemu ya tunda la Roho. Maana hapo,utagundua ya kwamba upendo wetu hukua na kuongezeka pale ufahamu wetu unapoongezeka kwa Mungu,kama ilivyoandikwa “ Na hii ndiyo dua yangu, kwamba pendo lenu lizidi kuwa jingi sana, katika hekima na ufahamu wote; “Wafilipi 1:9

03. UBATIZO.

Ubatizo ni moja ya sababu ya msingi sana ya ukuaji wa kiroho. Katika ubatizo ndipo mahali pekee tunapouzika utu wa kale na kufufuka na Bwana Yesu (Warumi 6:4). Ukweli ni kwamba bila ubatizo hujafanyika mkristo,na ikiwa hukufanyika mkristo basi ni dhahili huwezi kukua kiroho nje ya Kristo.

▪ Zipo haina mbili za ubatizo zinazoelezewa katika biblia,nazo ni;

(a) Ubatizo wa maji.

(b)Ubatizo wa Roho mtakatifu.

(a)Ubatizo wa maji mengi.( Baptism for salvation )

~ Ubatizo wa maji ni karamu inayofanyika kwa kuingia kwa mwamini katika kundi la kanisa. Ubatizo huu ni wa umuhimu sana,lakini ubatizo huu pekee hautoshi kumuokoa mwanadamu. Kuokolewa kunahitaji neema ya Mungu kwa njia ya imani kwa kumkiri BWANA YESU KRISTO na kumpokea,katika neema hiyo sasa kutembea katika utii wa Mungu.

Ubatizo huu unaweza kufananishwa na kutahiriwa kwa wana wa Israeli ambapo kwa tendo hilo la kutahiriwa kwao kuliwafanya waingie katika agano na kuanza kuhesabiwa kama wana wa Mungu.

Kumbuka hili,kukua kiroho kunahitaji hatua hii ya awali maana katika ubatizo huu ndipo maahali tunatimiza haki yetu ya msingi. (Mathayo 3:15). 

Yesu mwenyewe alibatizwa kutuonesha kielelezo cha ukuaji wa imani yetu na vile tupasavyo kuishi. Bwana Yesu anatuonesha ya kwamba Yeye pia alibatizwa katika ubatizo wa maji mengi. Imeandikwa;“Naye Yesu alipokwisha kubatizwa mara akapanda kutoka majini; na tazama, mbingu zikamfunukia, akamwona Roho wa Mungu akishuka kama hua, akija juu yake;“Mathayo 3:16

Neno “akapanda kutoka majini” linatupa picha kwamba Bwana Yesu alizama katika maji. Huwezi kupanda katika maji ikiwa hukuzama katika maji. Yeye apandaye ni yule aliyezama. Kumbuka pia Roho wa Bwana naye anahusika katika ubatizo wa maji,maana pasipo Yeye sisi hatuwezi kufanya lolote lile. 

(b)Ubatizo wa Roho mtakatifu (holy spirit baptism)

~ Ubatizo huu ni wa utofauti sababu Roho mwenywe hushuka na kumwaga karama zake kwa yule anayebatizwa. Ishara moja wapo ya uvuvio wa Roho mtakatifu ni kupokea nguvu (Matendo1:8),kisha kufuatana na kunena kwa lugha mpya (Matendo 2:1-4). Mitume hawakufanya lolote nje,mpaka walipopokea ahadi ya ujazo wa Roho mtakatifu. Hivyo utaona kuwa unahitaji pia ubatizo huu kwa afya yako ya roho.

TOFAUTI KATI YA UBATIZO WA MAJI MENGI NA UBATIZO WA ROHO MTAKATIFU;

~Nimejaribu kukupa tofauti tatu za msingi ambazo zitakusaidia katika imani yako kwa kipindi hiki unachohitaji kukua kiroho.

(i) Ubatizo wa Roho mtakatifu ni ahadi (Matendo 1:4-5). Wakati ubatizo wa maji sio wa ahadi bali ni wa lazima (Marko 16:16)

(ii) Ubatizo wa Roho mtakatifu husubiri muda wa BWANA vile atakavyo Roho (Matendo 1:4,6). Bali ubatizo wa maji hausubiri,bali wenyewe hufanywa pale tu mwamini anapoamini akifundishwa kwa usahihi habari za Yesu Kristo (Matendo 8:31-38)

(iii) Ubatizo wa Roho mtakatifu hufanywa kwa wachache wale waliokusudiwa na Roho mtakatifu ( Matendo 1:2-5,na 2:1-4). Ubatizo wa maji ni wa kila aaminie (Matendo 2:37).

▪ Hivyo,ubatizo kwa ujumla unakufanya ukamilishwe katika wokovu wako,na ndipo mahali haswaa unapokuwa kiroho…

ITAENDELEA

~Ikiwa kama unahitaji maombi na kuongea nami moja kwa moja,basi usisite kunipigia kwa namba yangu hii +255 683 877 900.

What’s app+255 746 446 446

Na Mch.Gasper Madumla.

UBARIKIWE.

Comments


Post: MAFUNDISHO

Follow

  • Facebook
  • Twitter

©2022 by MAFUNDISHO YA NENO LA MUNGU. Proudly created with Wix.com

bottom of page