top of page

KUKUA KIROHO? ~ 04


Mch.Madumla.

Mchungaji Gasper Madumla.


Bwana Yesu asifiwe…

Karibu tuendelee…

05. ONGEZA KIWANGO CHAKO CHA UTII KWA MUNGU.

Kadri unavyokuwa mtiifu kwa mambo yote ya Mungu ndivyo ukuaji wako wa kiroho huongezeka. Ni muhimu sana kuishi maisha ya utii lakini ikiwa utashindwa kuwa mtii mbele za Mungu,huwezi kukua kiroho hata iweje. Tena,kumbuka hili mtu yeyote asiyetii kweli ya Mungu kamwe hawezi kuongozwa na Roho mtakatifu,hivyo jambo lenye maana sana kwako ni kuishi maisha ya utii. Kwa sababu katika kuitii kweli ya Mungu kuna kuinuliwa,kuna kibali,kuna msaada utokao kwa Mungu,kuna kupendwa,kuna ushindi maana Bwana atakupigania, N.K

Waamini wengi wamenaswa katika eneo hili la utii kwa Mungu,wameshindwa kusikia sauti ya Mungu na kutii tena hujikuta wakidumaa kiroho kwa miaka mingi hali wameokoka.

Neno “utii kwa Mungu” ni neno pana sana lenye kukutaka kwanza kuisikia sauti ya Mungu inayosema nawe kwa njia tofauti tofauti haswa kwa kupitia watumishi wa Mungu ambao wamewekwa maalumu kwa ajili yako.Lakini pili kuyafanyia kazi yale yote uagizwayo,na huo ndio utii.

~Ukweli ni kwamba kukua kiroho hutegemea kiwango chako cha utii kwa Mungu. Ikiwa utaitii sauti ya Mungu kweli kweli,basi ni dhahili utakuwa na ongezeko kubwa la roho yako.

Utii ni kuweza kuisikia sauti ya Mungu na kuifanyia kazi sawa sawa na yote akuagizavyo BWANA Mungu wako. Bwana Yesu BWANA wa utukufu anatufundisha na kutupa kielelezo cha namna ya kuishi maisha ya utii kwa Mungu,maana Yeye ndio mwanzilishi wa imani yetu (Waebrania 12:2).

Tazama utii tunaojifunza kupitia Bwana Yesu,Biblia inasema;“na, ingawa ni Mwana, alijifunza kutii kwa mateso hayo yaliyompata; naye alipokwisha kukamilishwa, akawa sababu ya wokovu wa milele kwa watu wote wanaomtii; kisha ametajwa na Mungu kuwa kuhani mkuu kwa mfano wa Melkizedeki. “ Waebrania 5:8-10

Kumbuka pia Yeye Bwana Yesu alinyinyenyekeza akawa mtii hata mauti naam mauti ya msalaba. Kwa utii wa Yesu,Mungu alimwadhimisha mno na kumkirimia jina lipitalo kila jina,jina la Yesu Kristo ( Wafilipi 2:8-9). Hivyo kwa habari njema za Bwana Yesu,neno utii kwake lilikuwa kipaumbele chake,na ndio maana tunaona Yesu akiyatenda yote yale tu aliyoyasikia kwa Baba yake Mungu,na yote aliyoelekezwa. (Yoh.5:19).

▪ Kwa njia ya utii,ndipo tunafanana na Yesu Kristo.

~Tukihitaji kufanana na Bwana,hatuna budi kuishi maisha ya utii kwa MUNGU kama vile Yesu alivyokuwa mtii kweli kweli. ~Kumbuka mtu mtiifu hupendwa na Mungu,hata ukichukulia mfano wa kawaida kabisa~ukiwa na mtoto mwenye kukutii hakika utampenda hata yeye asipokuambia umpende lakini utatokea kumpenda. Kile kinachokusukuma umpende ni ule utii uliokuwa ndani yake.

▪ Utii ni bora kuliko dhabihu.(1 Samweli 15:22)

Mungu hupendezwa sana na utii wetu kwake zaidi ya matoleo tunayomtolea huku tukiwa wakaidi. Kinyume cha kutii ni kuasi,kukaidi. Wapo watu makanisani leo wanye kushika namba moja au wapo katika tano bora za utoaji lakini hali si watii kwa Mungu.

Maana utakuta Bwana Mungu ameagiza kwa watu wasizini,wasiibe lakini watu hawatii ile sauti na watu hao hao ndio wakwanza katika kuleta dhabihu mbele za Bwana. Tukiwa watu wa namna hii,basi kweli haipo mioyoni mwetu,kisha tutafanana na Sauli aliyeambiwa na MUNGU lakini hakutii ile sauti. (1 Samweli 15:1-35)

Shida iliyopo leo yenye kuzuia waamini wengi wasikue kiroho ni kushindwa kutii sauti ya Mungu. Ikiwa Mungu amesema nawe kwa habari ya kuacha maovu fulani,kwa njia ya mtumishi wake pale unapoabudu na ukikataa basi unakuwa sio mtii na hapo huwezi kukua kiroho maana inakuwa hujamkataa mtumishi wa Mungu bali umemkataa Mungu mwenyewe.

Tazama,mara ngapi mchungaji wako amesema na wewe kuhusu kulipa fungu la kumi,lakini mbona umekataa,je wewe ni mtii? Sasa Utakuwaje kiroho? Au mara ngapi mtumishi wako amekusisitiza uje kanisani kuhudhulia vipindi vya neno la Mungu na maombi yanayoendelea nawe ukasema “ niko bize sana,siwezi kuja kabisaa” tena utakuta mtu mwingine  kwa sababu amepata smart phone basi hudiliki kusema“nitumie mafundisho hayo katika whatsApp yangu mimi nitajisomea maani sina muda wa kuja huko!!!” Jiulize huu ndio utii?

Ifike wakati tuwe watii kwa habari ya mambo yote ya Mungu ili tuweze kukua kiroho zaidi…

ITAENDELEA…

~Ikiwa utahitaji maombi,basi usisite kunipigia kwa simu yangu hii;+255 683 877 900

What’s app number ni +255 746 446 446

Na Mch.Gasper Madumla.

UBARIKIWE.

Comments


Post: MAFUNDISHO

Follow

  • Facebook
  • Twitter

©2022 by MAFUNDISHO YA NENO LA MUNGU. Proudly created with Wix.com

bottom of page