BORA KUTESEKA MIKONONI MWA MUNGU,KULIKO KUPATA RAHA MIKONONI MWA SHETANI.
- Mch. Gasper Madumla
- Aug 26, 2014
- 2 min read

Bwana Yesu asifiwe …
Kwa ufupi.
Kuwa mikononi mwa Mungu haina maana hakuna mateso. Mateso yapo pia katika Bwana,utakutana nayo tu kwa sababu hata Yesu aliteswa; Na ndio maana Neno linatuambia kwamba wale wote wapendao kuishi maisha ya utauwa,wataudhiwa ( 2 Timotheo 3:12). Lakini ni afadhali sana kupitia mateso ukiwa mkononi mwa Bwana, kwa maana kuna ushindi utakaoupata kuliko kule kwa shetani.
Najaribu kuyatafakari maisha ya Musa pale alipokuwa akiishi kwa Farao kama mtoto wake. Musa alipozaliwa, alikulia kwenye kasri/ jumba la Farao lenye watumwa wa kila namna. Alikaa huko, na akasomeshwa Elimu ya Kimisri, na ukumbuke Misri ilikuwa ni sehemu iliyoendelea kiustaarabu/ yenye maendeleo lakini kulikuwa hakuna Mungu wa kweli bali waabudu sanamu, na wanajimu /wabashiri ndio walikuwa wengi huko.
Biblia inatuambia kwamba ; “Kwa imani Musa alipokuwa mtu mzima, akakataa kuitwa mwana wa binti Farao; akaona ni afadhali kupata mateso pamoja na watu wa Mungu kuliko kujifurahisha katika dhambi kwa kitambo;” Waebrania 11:24-25
Ilifika wakati ambapo Musa hakuona thamani kuendelea kuishi pamoja na Farao, maana walikuwa ni wenye miungu. Alipokuwa mtu mzima alifanya maamuzi magumu ya kutoka kwa Farao kwa kukubali kuteseka, lakini kuteseka akiwa mikononi mwa Mungu. Kwa sababu ndani ya kasri la Farao hakukuwa na mateso yoyote dhidi yake. Biblia inaanza kutuambia aliwezaje kutoka kwenye raha lakini ni kwa watenda dhambi “ kwa imani,… Alipokuwa mtu mzima… ”
Bila shaka Musa alikuwa na imani kwa maana imani hiyo ndiyo ilikuwa a driving force/ ilimsukuma kutoka. Kumbuka Musa alichaguliwa na Mungu lakini bado ilimlazimu kuyakubali mateso kwa ukombozi wa watu wa Mungu. Wewe pia umechaguliwa na Mungu, lakini je upo tayari kubeba msalaba au upo tayari kuendelea kujifurahisa na hao watenda dhambi?
Ni vyema kufahamu kuwa ni bora uteseke pamoja na Bwana kuliko kupata raha pamoja na watenda dhambi. shetani anaweza kukufanya usikie raha kwenye dhambi fulani, na kuona mambo yako yakiendelea kufanikiwa pasipo kujua, shetani huyo huyo ndiye nkuangamiza kwa siri nawe hujui.
Siku zote dhambi huonekana ni tamu kwenye mwili wako. Hata pale unapoambiwa uokoke, unaona kana kwamba ni uongo uongo fulani hivi, kwa sababu upo mkononi mwa shetani. Ukumbuke, kwamba maisha yetu wanadamu si marefu hivyo, ni mafupi kiasi kwamba hujui hata kesho yako utakuwa wapi. Ni vyema kama kuteseka, uteseke sasa ukiwa upande wa Mungu kwa maana mateso ya mtu wa Mungu yana msaada mkubwa wa Mungu ambaye Yeye ni mwaminifu, hatamwacha ajaribiwe kupita awezavyo na pamoja na mateso hayo, Mungu atafanya mlango wa kutokea.
Kwa msaada zaidi, pamoja na maombi piga sasa+255 683 877 900
Whastapp namba .+255 746 446 446
Mch. G. Madumla
UBARIKIWE.
Comments